WAJUMBE
wa Bunge Maalumu, wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), wamesema
hawatarudi bungeni na badala yake kuanzia kesho wataanza mikutano ya hadhara
nchi nzima kuwaeleza wananchi juu ya hila za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na
washirika wake kutaka kuhodhi mchakato wa uandikaji wa Katiba mpya.
UKAWA
wamesema katika mikutano hiyo watazisambaza ‘CD’ zinazomuonesha Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, akiwa katika
Kanisa la Methodist, mkoani Dodoma akiwaeleza waumini wakatae muundo wa
serikali tatu.
Walisema
kwenye CD hizo, Lukuvi, anaonekana akiwaambia wananchi iwapo wataridhia muundo
wa serikali tatu, jeshi litachukua nchi na Zanzibar itaingia katika utawala wa
Kiislamu.