Thursday, April 17, 2014

HATUTARUDI BUNGENI NG'O!!!!!!!NI KAULI YA UKAWA,,WAJIPANGA KUSAMBAZA CD ZA HOTUBA YA LUKUVI KANISANI NCHI NZIMA.


WAJUMBE  wa Bunge Maalumu, wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), wamesema hawatarudi bungeni na badala yake kuanzia kesho wataanza mikutano ya hadhara nchi nzima kuwaeleza wananchi juu ya hila za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na washirika wake kutaka kuhodhi mchakato wa uandikaji wa Katiba mpya.
UKAWA wamesema katika mikutano hiyo watazisambaza ‘CD’ zinazomuonesha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, akiwa katika Kanisa la Methodist, mkoani Dodoma akiwaeleza waumini wakatae muundo wa serikali tatu.
Walisema kwenye CD hizo, Lukuvi, anaonekana akiwaambia wananchi iwapo wataridhia muundo wa serikali tatu, jeshi litachukua nchi na Zanzibar itaingia katika utawala wa Kiislamu.

Juzi wajumbe wa UKAWA walisusia kikao cha Bunge Maalumu kwa madai ya kuchoshwa kusikiliza matusi, ubaguzi na kauli za chuki zinazotolewa na wajumbe kutoka CCM bila viongozi wakubwa kukemea.
Jana wakizungumza na waandishi wa habari, viongozi wa UKAWA walisema hawatarejea bungeni mpaka watakapoketi 
Jana wakizungumza na waandishi wa habari, viongozi wa UKAWA walisema hawatarejea bungeni mpaka watakapoketi kwenye vikao vya maridhiano ambavyo pia watakwenda na masharti yao mojawapo ni rasimu ya Tume ya Warioba ndiyo iwe msingi wa majadiliano.
Masharti mengine ni kukaa kwenye meza ya maridhiano na viongozi wa serikali na CCM, kusiwepo matusi, ubaguzi na kauli za chuki.
Mmoja wa viongozi wa UKAWA, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema kuwa watazunguka nchi nzima kuwaeleza wananchi kilichotokea bungeni na namna CCM wanavyopenyeza rasimu yao kwa mlango wa nyuma.
“Sisi tupo tayari kwa mazungumzo kama tulivyoombwa na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta, lakini hatutakubali kubeba matakwa ya CCM, tunataka tujadili rasimu ya Tume ya Jaji Warioba ambayo ilikwenda kuwahoji wananchi,” alisema.
Profesa Lipumba, alisema wameamua kususa vikao vya Bunge kwa sababu hawako tayari kushiriki kupitisha masuala yenye masilahi ya CCM yaliyopelekwa bungeni kwa mlango wa nyuma.
Alisema walitegemea wajumbe wangejikita kujadili rasimu iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa hoja lakini badala yake wameshuhudia matusi, ubaguzi, kauli za chuki ambazo zinachangia zaidi kuligawa taifa.
Lipumba alisema rasimu iliyopo mezani inataja serikali tatu hivyo kama wajumbe wa CCM wanataka kujadili serikali mbili, lazima Bunge livunjwe na iundwe tume nyingine itakayotoa rasimu ya serikali mbili.
“Wenzetu wanatushangaza sana yaani walivyokuwa wakijadili rasimu ile kama imetolewa na wapinzani, hii ni rasimu iliyotolewa na tume iliyoundwa na rais, sasa kama wenzetu hawaamini sisi tunakwenda kuwaeleza wananchi CCM isivyotaka kuandika Katiba yenye masilahi ya wananchi,” alisema.
Lipumba pia alisema Chama cha Wananchi (CUF), kitaangalia hatua za kisheria za kumchukulia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alivyokihusisha chama hicho na taasisi ya kidini ya UAMSHO.
Alisema si kweli kwamba CUF imekuwa ikishirikiana na taasisi hiyo ambayo mara kadhaa imekuwa ikihusishwa na mihadhara ya kidini yenye vurugu visiwani Zanzibar.
Naye James Mbatia, alisema maridhiano ndiyo yatakayosaidia mchakato wa Katiba kusonga mbele lakini kwa hali inavyoonekana CCM hawana dhamira ya kuandika Katiba yenye kujali masilahi ya wananchi.
Alisema wiki iliyopita TCD iliitisha mkutano wenye lengo la kutafuta maridhiano lakini CCM walituma wawakilishi wasio na nyadhifa za juu kama zilivyofanya pande nyingine.
Naye Mwenyekiti wa UKAWA, Freeman Mbowe, alisema wameamua kususa vikao vya Bunge kwakuwa wajumbe wengi kutoka CCM wameacha kujadili rasimu iliyowasilishwa na Tume ya Warioba ambayo ndiyo msingi wa majadiliano yao.
Alisema Tume ya Warioba iliwekwa kisheria na ilifanya kazi ya kuwahoji watu pamoja na kutumia nyaraka mbalimbali hadi kufikia kutoa rasimu isiyotakiwa na wajumbe wa CCM walioanza kujadili rasimu waliyopewa na chama chao.
“Kususia vikao vya Bunge ni miongoni mwa hatua za kutafuta haki, kuendelea kushiriki vikao hivi ni kuhalalisha na kubariki udhalimu wa CCM ambayo imeamua kukwamisha Katiba mpya.
“Matusi, ubaguzi, chuki haviwezi kutusaidia kupata Katiba mpya, UKAWA hatuko tayari kuendelea kushiriki majadiliano yenye mambo hayo….tunakwenda kwa wananchi kuwaeleza kile kinachofanywa na wajumbe humu bungeni,” alisema.
Mbowe alisema si lazima Rais Jakaya Kikwete aondoke madarakani wakati Katiba mpya imepatikana bali mchakato huo unaweza kuendelezwa na rais mwingine lakini katika mazingira yanayokubalika na watu wote.
Posho
Hata hivyo wajumbe wa Katiba, walikuwa wakipigana vijembe kuwa UKAWA wameamua kususa vikao vya Bunge baada ya kulipwa posho ya vikao mpaka Aprili 22 mwaka huu.
Said Nkumba, alisema UKAWA ni wanafiki kwakuwa wamesusia vikao hivyo baada ya kulipwa fedha hizo na kama wasingelipwa wasingethubu kulikimbia Bunge.
Livingstone Lusinde, alisema UKAWA, hawana ujasiri wa kutetea masilahi ya umma bali wapo kwa ajili ya kuangalia masilahi binafsi ndiyo maana waliondoka bungeni baada ya kusikia wamelipwa fedha mpaka Aprili 22.
Naye Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Mwigulu, Nchemba, alisema jana waliwasiliana na benki kuona kama zilikuwa zimefanya malipo kwa wajumbe hao wazuie fedha hizo ili kuwadhibiti wajumbe wa UKAWA ambao wanachukua fedha bila kufanya kazi
Hata hivyo kauli hiyo ilionekana kupinga na Katibu wa Bunge, Yahya Khamis, aliyesema fedha hizo tayari zimeshaingizwa kwenye akaunti za wajumbe.
Khamis, alisema kuanzia Aprili 22, ndiyo watajua kama wajumbe wa UKAWA, hawatahudhuria vikao vya Bunge  hawataingiziwa fedha za kujikimu na ile ya vikao.
Kwa siku moja wajumbe hao wanalilipwa sh 300,000 ambapo sh 230,000 ni posho za kujikimu, sh 70,000 posho ya vikao.
Makatibu Wakuu UKAWA watoa kauli
Makatibu wakuu wa UKAWA wamesema wabunge wao hawatarejea bungeni badala yake watazunguka nchi nzima kuelezea namna serikali ya CCM isivyotaka wananachi wapate katiba wanayoitaka.
Mbali ya msimamo huo, pia wameeleza mbele ya waandishi wa habari kuwa kuwa Rais Jakaya Kikwete alipopata fursa ya kulihutubia Taifa wakati wa kulizindua bunge, alianzisha vita ya kisiasa na kuigawa nchi vipande kutokana na vitisho alivyovitoa kama mkuu wa nchi.
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilbroad Slaa, alisema wao kama makatibu wakuu wanaunga mkono wabunge wao kutoka nje na kukiita kitendo hicho kuwa ni  cha kishujaa na uzalendo wa kukataa kuburuzwa.
Alisema hakuna chama kinachotaka Katiba Mpya kwa dhamira ya kuvunja muungano kama wanavyodai CCM, badala yake wanataka katiba ya maridhiano yanayoongozwa na uamuzi wa wananachi.
“Haya ni mapambano  na vita inayohitaji kuunganisha nguvu zote kwa kuwa hili ni jambo kubwa kwa mustakabali wa taifa na tunapoona watu wanafanya masikhara kwa ajili ya masilahi na misimamo ya vyama vyao, hatuwezi kukubali,” alisema Dk. Slaa.
Aliongeza kuwa kuna hatari ya mfumo uliozaa katiba inayotumika sasa kurejeshwa katika mfumo mzima wa upatikanaji wa katiba mpya na kwamba kama vyama vya siasa walionya hali hiyo mapema kwa ajili ya kulinda umoja wa kitaifa.
“Tulikuwa tayari kuridhiana kuanzia mwanzo lakini wenzetu hawataki maridhiano zaidi ya misimamo yao inayolindwa na wingi wao ndani ya bunge, sasa sisi tuna watu nje ya bunge na kama wanasema kuwepo kwa serikali tatu jeshi litapindua nchi huo ni uongo, kama mapinduzi yangefanyika sasa kwa kuwa wamewadhulumu hao wanajeshi hata hela zao za Operesheni Tokomeza,” aliongeza Dk. Slaa.
Dhana ya Vitisho
Kaimu Katibu Mkuu wa CUF, Shaweji Mketo, alisema ni jambo la kusikitisha kuona serikali inatumia vitisho kwa wananchi wakati walibariki mchakato mzima wa kukusanya na kuandika maoni ya wananchi ya kupatikana katiba mpya
Mketo alisema kitendo cha wabunge wao kutoka nje kilitosha kulivunja bunge kwani rasimu haisemi mjadala wa serikali mbili.
UKAWA haitarudia makosa
Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR Mageuzi, Mosena Nyambabe, alisema kulikuwa na makosa mengi wakati vyama vya siasa viliporidhia kuingia kwenye mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 bila kupata katiba mpya.
Alisema hoja zinazotolewa kuwa wapinzani hawataki katiba mpya zinapotoshwa makusudi, kwa kuwa madai ya vyama vya upinzani kuhusu katiba ya wananachi yalianza miaka ya 1960.


No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...