mgombe ubunge kupitia CCM jimbo la kalenga bwana Godfrey Mgimwa akiwa na katibu wa ccm wilaya ya Mufundi
KATIBU wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mufindi, Miraji
Mtaturu amewataka wananchi wa Jimbo la Kalenga kujua kiasi cha fedha anazolipwa
Dk Wilbroad Slaa kila mwezi ili waoanishe na harakati zake anazodai zinalenga
kupinga ufisadi.
Dk Slaa ni Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (Chadema); yupo wilayani Iringa akiongoza kampeni za kumnadi Grace
Tendega anayegombea ubunge katika jimbo hilo kupitia chama hicho.
Katika mikutano ya kumnadi mgombea wao Godfrey
Mgimwa iliyofanyika katika vijiji vinne vya kata ya Kiwele jana, Mtaturu
alisema Dk Slaa ndiye kiongozi wa chama cha siasa nchini anayelipwa fedha
nyingi kuliko mwingine yoyote.
Alisema katika mazingira ambayo wanachama na
baadhi ya viongozi watendaji wa Chadema wanatumia fedha zao za mifukoni kujenga
chama hicho, Dk Slaa analipwa zaidi ya Sh Milioni 10.
“Muulizeni akija hapa ni kiasi gani analipwa
kila mwezi; aliwekwa sharti la kulipwa kiwango kinachofanana na kile
wanacholipwa wabunge kama sharti la kukubali kugombea urais badala ya ubunge
katika Uchaguzi Mkuu uliopita,” alisema.
Alisema mtu anaweka masharti na kutanguliza
maslai yake mbele katika kazi ya kuwatumikia wananchi hafai kuwa kiongozi na ni
muhimu kuwa makini na kauli zake.
Katika mikutano iliyofanyika katika vijiji vya
Mgera, Kiwele, Mfyome na Kitapilimwa, Mtaturu aliwaomba wananchi wa jimbo la
Kalenga kutofanya makosa katika uchaguzi huo.
“Kazi anayokwenda kumalizia Godfrey Mgimwa
ilikwishaanza kufanywa na marehemu Dk William Mgimwa; mpeni kura zenu zote ili
akamalizie utekelezaji wa Ilani ya CCM,” alisema.
Akijinadi kwa wapiga kura wa kata hiyo, Mgimwa
alisema “sijagombea nafasi hii ili niharibu kazi inayoendelea kufanywa na chama
changu, sikugombea ili kupotosha ukweli wa yale yote yanayoendelea
kufanywa, ninagombea kwasababu nataka
kumalizia kazi,” alisema.
Alisema akiwa mbunge katika jimbo hilo
atahakikisha kwa kushirikiana na wapiga kura wake anamalizia utekelezaji wa
ahadi mbalimbali za maendeleo zilizotolewa na CCM kupitia Ilani yake ya 2010 na
zile zilizoachwa na marehemu baba yake.
“Najua katika kata hii kuna changamoto
zinazoendelea kupatiwa ufumbuzi; nipeni nafasi nikazishughulikie,” alisema na
kuzitaja changamoto hizo zikihusisha sekta ya maji, afya, barabara, pembejeo,
elimu na mawasiliano.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Iringa, Delfina
Mtavilalo alisema katika uchaguzi huo Chadema itashika nafasi ya pili kama
inavyojidhihirisha kupitia salamu yao.
“Vidole viwili havina maana nyingine zaidi ya
namba mbili na ndio maana kila wanapopita wanaonesha wao ni namba mbili kwa
kuonesha ishara ya vidole hivyo,” alisema.
Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa, Hassan Mtenga
alisema wananchi wa Kalenga watakosea kama watampa ubunge mtu ambaye hawajui
watampata wapi.
Alisema CCM inawajibika kwa wananchi na ndio
maana ina mfumo wa uongozi kutoka ngazi ya tawi hadi taifa tofauti na Chadema.
Akiahidi kutoa zawadi ya fedha kwa wananchi wa
kata ya Kiwele kama watamtajia safu ya viongozi wa chama hicho katika jimbo
hilo, Mtenga alisema bado hakiaminiki na ndio maana kinakosa viongozi katika
nafasi zake mbalimbali.
“Ulizeni kama kina viongozi wa kuchaguliwa
kwenye kata zake na kama kina uongozi wa wilaya uliokamilika,” alisema.
No comments:
Post a Comment