Tuesday, August 27, 2013

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema kinakubaliana na rasimu ya Katiba kwa sababu asilimia 80 ya rasimu hiyo kwa kile inachoeleza inalinda maslahi ya wananchi.Kadhalika Chama hicho kimependekeza kuingizwa kwa kipengele cha haki ya wakulima na wafugaji katika Katiba mpya huku, kikiunga mkono kuwapo kwa serikali tatu .

Hayo yalisemwa na Katibu Mkuu wa chama hicho,Wilbroad Slaa, wakati akiwahutubia wananchi wa wilaya ya Mkuranga, mkoa wa Pwani, katika kampeni ya kukusanya maoni ya wananchi kuhusu Katiba mpya.
Slaa alisema Chadema inaunga mkono kuwapo kwa serikali tatu kama ilivyopendekezwa na Tume ya Mabadiriko ya Katiba mpya inayoongozwa na Jaji Mstaafu Joseph Warioba.
“Tunakubalina na Tume ya Warioba kwa asilimia 80, lakini tunatofautiana naye kwa asilimia 20, kitabu chake tunakipokea, na hoja zake tunazipokea, lakini yeye hatumkubali kwa kuwa ni kibaraka wa CCM,” alisema Slaa.
Kadhalika Slaa alimtaka Jaji Warioba kuhakikisha katiba mpya inasimamia haki, na kukemea vitisho, rushwa, na unyanyaswaji kwa wananchi.
Alisema Chadema inaitaka kuiona Tanzania kuwa nchi isiyo ya dhuluma huku utajiri na rasilimali zake ukihifadhiwa kwa maendeleo ya vizazi vijavyo.
Alisema Tume ya Jaji Warioba imechukua maoni ya Watanzania wengi na kuyaweka katika rasimu hiyo, lakini alitoa angalizo kwa tume hiyo kutoichakachua rasimu hiyo.
Baadhi wa wananchi wa Mkuranga walipata nafasi ya kutoa maoni yao huku wengi wakipendekeza kipengele cha Rais kushitakiwa pindi atakapoenda kinyume na utaratibu uliwekwa nchini.


No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...