Sunday, May 25, 2014

SUALA LA UJENZI WA KITUO CHA MABASI IGUMBILO,MANISPAA YA IRINGA YAGALAGAZWA,,so ni kama vile CDM WAMESHINDA ILE INDIRECT WAR.





WAZIRI WA TAMISEMI AKIFAFANUA JAMBO

















SERIKALI kuu imefanya maamuzi magumu yaliyoiachia halmashauri ya manispaa ya Iringa kilio chenye tiba baada kuzuia mpango wake wa kujenga stendi mpya ya mabasi yaendayo mikoani katika eneo linalolalamikiwa na wadau wa mazingira la Igumbilo, mjini Iringa.

Na wakati huo huo imeipoza halmashauri hiyo kwa kuwaahidi kuchangia gharama mbalimbali zitakazohitajika kufidia na kutathimini eneo mbadala watakalopata kwa ajili ya ujenzi huo.

Zuio hilo lililokunja sura za baadhi ya madiwani na watendaji wa manispaa hiyo “waliotaka kujua nani atafidia gharama zao walizotumia katika mchakato mzima wa ujenzi wa stendi hiyo” lilitolewa jana mjini Iringa kupitia matamko yaliyotolewa na mawaziri watatu tofauti.

Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, Waziri wa Mazingira, Dk Binilith Mahenge na Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia kwa pamoja walitoa ufafanuzi wa zuio hilo wakati wakizungumza na wanahabari ambao awali walizuiwa kuingia kwenye kikao kilichokuwa kikipokea taarifa hiyo.

Mbali na mawaziri hao, wajumbe wa baraza la madiwani la manispaa hiyo, sekretarieti ya mkoa wa Iringa, wawakilishi wa vyama mbalimbali vya siasa, Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na wadau mbalimbali wa mazingira na maji walihudhuria kikao hicho.

Akitoa taarifa ya zuio hilo huku akishangaa kwanini wanahabari walizuiwa kuingia katika kikao hicho, Waziri wa Tamisemi, Ghasia alisema tathimini ya pili ya athari ya mazingira iliyofanywa na NEMC inahalalisha maamuzi hayo.

Alisema NEMC ilifanya tathmini hiyo baada ya mdau namba moja wa eneo hilo linalopitiwa na mto Ruaha Mdogo, Wizara ya Maji kupinga ujenzi wa stendi hiyo huku ikianisha sababu mbalimbali.

Waziri Ghasia alisema mto huo ndiyo chanzo pekee kinachohudumia jamii nzima ya wananchi wa manispaa ya Iringa na hivyo kujenga stendi jirani yake kutaongza shughuli za kibinadamu zinazoweza kuathiri mto huo na mazingira yake na hatimaye wanufaika wake.

Kwa kupitia mto huo serikali kwa kupitia Mamlaka ya Maji Safi na Majitaka Iringa (IRUWASA) imewekeza zaidi ya Sh Bilioni 70 ili kuwapatia wananchi maji safi na salama. Mradi huo ulizinduliwa na Rais Jakaya Kikwete Machi 22, 2012.

Ni katika mto huo (mita kadhaa kutoka katika eneo linalopendekezwa kujengwa stendi) kuna mitambo ya IRUWASA ya kupokea, kusafisha na kusambaza maji katika mji wa Iringa.

Alisema taarifa iliyopo inaonesha kwamba ujenzi wa stendi hiyo utakwenda sambamba na ujenzi wa huduma zingine zikiwemo gereji, hoteli na maduka hali inayoweza kuhatarisha mazingira na usalama wa maji yam to huo.

“Kwahiyo tumewaeleza rasmi ndugu zetu wa manispaa kwamba stendi hiyo haitajengwa katika eneo hilo lakini kwakuwa wanayo mipango ya ujenzi huo utakaofadhiliwa na Benki ya Dunia, watafute sehemu nyingine,” alisema.

Alisema serikali inatambua gharama ambazo manispaa hiyo imeingia tangu ianze mchakato huo mwaka 2008 na ili kuponya machungu hayo itawajibika kutoa fedha zitakazohitajika kwa ajili ya kuandaa eneo mbadala.

Naye Dk Mahenge alisema; “sio jambo la ajabu kwa serikali kubadili maamuzi iliyoyafanya awali, tumeamua hivyo baada ya kubaini kuwepo kwa baadhi ya mambo ambayo hayakuzingatiwa wakati tathimini ya awali ikifanywa, mambo hayo ni pamoja na athari za mabadiliko ya tabia nchi zinazoweza kutokea katika eneo hilo.”

Tathimini hiyo ya awali ilifanywa na Mtaalamu Mshauri wa Mazingira aitwaye Arms on Environemnt Ltd ya Dar es Salaam kwa gharama ya zaidi ya Sh Milioni 25 kama ilivyoelezwa katika cha Kamati ya Fedha na Uongozi  kilichofanyika Mei 2011.

Profesa Maghembe alisema kumbukumbu zinaonesha kuwepo kwa mvutano wa ujenzi wa stendi hiyo tangu mchakato wake uanzishwe mwaka 2008 kwahiyo kilichofanywa na serikali ni kwa faida ya wananchi na Taifa kwa ujumla wake.

Dk Mahenge alisema Oktoba mwaka jana na Februari 19 mwaka huu alipata malalamiko ya kimaandishi kutoka kwa mdau namba moja wa maji ambaye ni Wizara ya Maji, akionesha hofu ya wadau mbalimbali wa maji na mazingira endapo stendi hiyo itajengwa hapo.

Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa alisema: “Suala hili sio la kisiasa hata kidogo, ni suala la maendeleo ya watu, kwahiyo tuipongeze serikali kwa kuzingatia ushauri uliotolewa na wataalamu wake, haya ndio maendeleo.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa, Amani Mwamwindi alikataa kutoa mtazamo wake baada ya kupokea uamuzi huo hata hivyo Waziri Ghasia aliingilia kati na kuitaka halmashauri hiyo iendelee na mipango ya kujenga stendi kwa kutafuta eneo lingine.

Kuzuiwa kwa ujenzi huo, kulitabiriwa na wadau mbalimbali baada ya Februari mwaka huu, Dk Mahenge kutembelea eneo hilo na kuiagiza NEMC kufanya upya tathimini hiyo huku akiiagiza manispaa hiyo kusimamisha shughuli zote ilizokuwa imepanga kufanya katika eneo hilo.
    
Kwa mujibu wa taarifa ya Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringabaada ya tathimini  ya awali kuonesha hakutakuwepo na athari za mazingira kama stendi hiyo itajengwa katika eneo hilo, walipewa hati ya ujenzi Na.EC/E15/584 iliyotolewa Juni 15, 2012.




No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...